KPAH SHERMAN NI JEMBE



Mshambuliaji mpya wa Yanga, Kpah Sherman (kulia) akiwa na meneja wa timu hiyo, Hafidh Saleh mara baada ya kuwasili kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Dar es Salaam akitokea Cyprus jumatano 

STRAIKA matata wa Liberia, Kpah Sean Sherman, ametua Yanga Jumatano mchana tayari kwa mapambano, lakini ametoa angalizo kwamba atafanya yake ndani ya mwaka mmoja kisha asepe.
Mchezaji huyo aliyefunga mabao 24 kwenye Ligi Kuu Cyprus msimu uliopita, amewaambia viongozi wa Yanga kwamba hataki kufanya kazi muda mrefu Jangwani, ndiyo maana anataka mkataba mfupi.
Akizungumza baada ya kuwasili, Sherman alisema amefurahi kujiunga na Yanga na anataka kutumia nafasi hiyo kukabiliana na changamoto mpya katika maisha yake.
“Sijasaini mkataba wowote, lakini naamini kila kitu kitakuwa sawa baada ya kukutana na viongozi, nataka kupata changamoto mpya nikiwa hapa, sina wasiwasi na uwezo wa kutekeleza majukumu yangu uwanjani kwani ninaimudu vyema kazi yangu ya mshambuliaji,”alisema Sherman.
Kocha Msaidizi wa Yanga, Leonardo Neiva, amesisitiza kwamba straika huyo ni mtaalamu wa kufunga mabao na kazi yake kubwa ni kumalizia mipira golini na kupambana na mabeki. Aliongeza kwamba hawafanyi kazi kwa kubahatisha ndiyo maana wanasajili mtu wa maana atakayerudisha ubingwa wa Ligi Kuu Bara Jangwani na mwakani wafanye vizuri pia kwenye Kombe la Shirikisho ambalo Marcio Maximo amelipania.
Kocha huyo Mbrazili aliliambia Mwanaspoti kuwa hakutaka kusema lolote juu ya ujio wa mchezaji huyo pamoja na uwezo wake kwasababu alikuwa akichunguza kwa kina juu ya uwezo wake.
“Nimefuatilia binafsi na nimeona Sherman anajua kazi ya kufunga mabao, ni mchezaji mwenye umbile kama la Jaja (Genilson Santos), lakini yuko fiti na ana uwezo mkubwa wa kufunga,” alisema.
“Kwanza ana nguvu na kasi, pia anaweza kufunga kutoka eneo lolote kwa staili tofauti, anapiga mashuti makali, mjanja anapokabwa na ana soka la nguvu.”

Comments

Popular posts from this blog

JINSI YA KUKAA NA NGUVU ZA MUNGU SEHEMU YA KWANZA

MAGONJWA 27 YANAYOTIBIWA NA ASALI YENYE MDALASINI